Tuesday, July 24, 2012

SHAIRI LA RAMADHANI MWAKA 2012

KARIBU WETU MGENI, MTUKUFU RAMADHANI wa MWAKA 2012 (1) Salam zangu natuma, mijini na vijijini, habari imeshavuma, mgeni yupo njiani, mwezi kuandama, ni yetu matumaini, (2) Mwezi huu wa fadhila, na mwezi wa ihsani, sio mwezi wa chakula, kushindilia tumboni, au mwezi wa kulala, kukoroma kitandani, (3) Mwezi huu wa ibada, na kusoma Qur-aani, ni mwezi wenye faida, nyingi ziso na kifani, sio mwezi wa kawaida, ni mwezi wenye thamani, (4) Imo siku ya Kudura, kwenye kumi za mwishoni, hiyo siku ndio bora, kuliko zote yakini, ni siku yenye kung'ara, Jibrili ni mgeni (5) Mwezi huu mashetani, wana pingu mikononi, minyororo ya shingoni, wametiwa huwaoni, Ona vipi Rahmani, mwezi Anauthamini! (6) Mwezi huu Qur-aani, ilishuka ardhini, kwa wahyi toka mbinguni, ni maneno ya Manani, isomwe kila makani, itunawiri moyoni, (7) Mwezi huu tarawihi. ni Swalah za Ramadhani usikose kuziwahi, ziswali msikitini, mwenyewe utafurahi, utakuwa burudani (8) Mwezi huu mafakiri, pamoja na masikini, uwaalike futari, wakaribishe nyumbani, wape maneno mazuri, na sadaka mkononi, (9) Mwezi huu wa kufunga, kila kitu mdomoni, sio mwezi wa kuringa, kujivuna mitaani, ni mwezi wa kujikinga, na maasi duniani (10) Mwezi huu kujishika, kujizuia mwilini, usiyavuke mipaka, yalokatazwa na dini, na ibada shughulika, asubuhi na jioni (11) Mwezi huu kula daku, mama aende jikoni, ukiingia usiku, kula unavyotamani, mchana ni marufuku, ila uwe safarini, (12) Mwezi huu inafungwa, milango yote motoni, hapo inafunguliwa, milango yote peponi, dua zinakubaliwa, ombeni ndugu ombeni (13) Mwezi huu wa kutubu, uyafute ya zamani, uzikusanye thawabu, uombe na samahani, uzungmze kwa adabu, na ndugu na majirani, 14) Mwezi huu tenda mema, uchoyo weka pembeni, tena uwe na huruma, kwa wale walioduni, kama Mungu kawanyima, huo ndio mtihani, (15) Mwezi huu wa baraka, wa amani na imani, Ninamuomba Rabuka, pepo iwe maskani, Ni mwisho wa kuandika,nimefika kikomoni, NAWATAKIA RAMADHANI NJEMA AMEEN.

No comments:

Post a Comment